
| Ham volume 8 - Jarida la mabadiliko na uimarishaji wa sekta ya Afya Tanzania (Wizara ya Afya, 1998, 38 p.) |
Na Filemon Lubuva
Nchi zinazoendelea huenda zikakabiliwa na matatizo makubwa zaidi siku za usoni, kutokana na kasi ya ongezeko la idadi ya watu wenye umri mkubwa.
Taarifa zinasema, kati ya watu 580 milioni wenye umri kati ya miaka 60 na kuendelea duniani, 355 milioni wanaishi katika nchi zinazoendelea ambazo wengine huziita nchi za Dunia ya Tatu.
La muhimu zaidi ni taarifa za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinazosema kuwa ifikapo mwaka 2020, watakuwepo ulimwenguni watu 10000 milioni wenye umri wa miaka 60 na zaidi, na 70 millioni kati yao wataishi katika nchi zinazoendelea.
Wataalam wa masuala ya idadi ya watu, wanasema tatizo la umri mkubwa linatokana na viwango vya vifo na uzazi kwa maana kwamba watoto wachache wanazaliwa na watu wengi zaidi wanafikia umri mkubwa.
Ongezeko la idadi ya wazee katika jamii, unamaanisha kwamba mataifa yatakuwa na jukumu kubwa zaidi la kuwalisha wazee hao pamoja na watoto ambao kimsingi hawana uwezo wa kufanya hivyo wenyewe.
Aidha, ina maana mataifa yatatakiwa kufanya jitihada kubwa zaidi kupanua uzalishaji wa chakula, kuongeza kiasi na ubora wa utoaji wa huduma za jarnii, na kuwa tayari kutoa huduma zingine muhimu kwa maisha na uhai wa binaadamu kwa kiwango cha kuridhisha.
Taarifa za kijarida cha Fact Sheet cha WHO, zinasema kumekuwa na kupungua kwa kiwango cha vifo katika nchi zinazoendelea kwa kipindi cha miaka 50 iliyopita, na hivyo kuongezeka kwawastaniwa matarajio ya kuishi baada ya kuzaliwa kutoka miaka 41 kwenye miaka ya hamsini hadi 62 mwaka 1990. Matarajio ya maisha katika nchi hizo yanatabiriwa kufikia miaka 70 mwaka 2020.
Miongoni mwa nchizinazoendelea zenye matarajio mazuri ya kuishi kiasi cha miaka 72 na kuendelea ni Costa Rica, Cuba, Jamaica na Argentina. Zingine ni Malaysia na Jamuhuri ya Korea.
Imesemekana kufikia mwaka 2020, kati ya nchi 10 zilizo na idadi kubwa ya watu wenye umri mkubwa, tano zitakuwa Dunia ya Tatu ambapo China itakuwa na watu 230 milioni, wengine 142 milioni watakuwepo India na 29 milioni Indonesia.
Nchi ya Brazil iliyopo Amerika ya Kusini na Pakistani katika Bara la Asia zitakuwa na jumla ya wazee wapatao 27 milioni na 18 milioni katika mpangilio huo huo.
Nchi zilizoendelea ziko katika nafasi nzuri zaidi kuhusiana na tatizo la kukua kwa umri, kwa sababu ya kupungua kwa uzazi, ubora wa hali ya maisha na maendeleo ya teknolojia katika nyanja za madawa ambayoyamewezesha kutengenezwa kwa madawa ya kufaa zaidi pamoja na dawa za chanjo.
Katika mataifa yanayoendelea, hali ni kinyume kwa vile uzazi unapungua kwa kasi zaidi wakati matarajio ya maisha yanaongezeka zaidi kutokana na huduma za hospitali kwa kutumia teknolojia ya hali ya juu.
Katika nchi ya Dunia ya Tatu, huduma hizi zimewezesha kutibiwa na kudhibitiwa kwa magonjwa mbalimbali ambayo hapo awali yalikuwa yanaua watu wengi wakati wangali wadogo.
Kuzorota kwa kiwango cha afya kiakili, pamoja na kukua kwa idadi ya watu wanaofikia umri wa hatari wa kuchanganyikiwa, ni matatizo mengine yanahusiana na kukua kwa umri.
Wakati ambapo hivi leo wapo watu wasiopungua 29 milioni wanasumbuliwa na magonjwa ya akili, takwimu zinaonyesha kuwa ifikapo mwaka 2020, idadi hiyo itaongezeka zaidi kufikia kiwango cha watu 55 milioni Barani Afrika, Asia na Amerika ya Kusini.
Wanasiasa na viongozi wengine muhimu katika jamii ambao mikononi mwao yamewekwa matarajio ya mamilioni ya watu katika nchi zinazoendelea, wanayo kazi kubwa kukabiliana na changamoto ya kukua kwa umri licha ya matatizo mengine mengi yanayozikabili nchi hizo.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopo, matatizo ya macho na kupoteza kabisa uwezo wa kuona ambayo yanahusiana pia na kukua kwa umri, yanaongezeka sana.Kiasi cha watu 45 milioni duniani ni vipofu na wengine 135 milioni wana uwezo hafifu wa kuona.
Tatizo la cataract linaelezwa ndilo lililosababisha watu 19 milioni duniani kupofuka na linahusishwa pia na asilimia 40% ya upofu Barani Afrika na Asia.
Hatua madhubuti inafaa zichukuliwe sasa kukabiliana na tatizo la kukua kwa umri. Kuzinduliwa kwa Mpango wa Kukua kwa Umri kulikofanywa na WHO mwaka 1995, ni mwanzo mzuri lakini kila nchi inabidi ifanye jitihada za maksudi na za dhati kuutekeleza.
Matokeo ya kijamii na afya ya jamii kuhusiana na kukua kwa umri hasa katika nchi zinazoendelea, vinatakiwa kuangaliwa kwa makini. Katika nyingi ya nchi hizo, umasikini, kukosekana kwa mipango ya usalama wa kijamii, kuendelea kukua kwa miji, na ongezeko la ushiriki wa wanawake katika kazi, vinachangia mmomonyoko wa njia za asili za kuwatunza watu wenye umri mkubwa, inasema taarifa ya WHO.

Furaha ya wazee na wajukuu
zake