
| Ham volume 8 - Jarida la mabadiliko na uimarishaji wa sekta ya Afya Tanzania (Wizara ya Afya, 1998, 38 p.) |
Imefahamika kuwa wilaya ya Makete Mkoani Iringa inaongoza Kitaifa kwa kuwa na watu wengi waliombukizwa virusi vya UKIMWI na hivyo kusababisha idadi ya watoto yatima kuongezeka.
Hayo yalizungumzwa na Mratibu wa Shirika moja lisilo la kiserikali lijulikanalo kama Tanzania Home Economics Association (TAHEA). Bi Lediana Mafuru, alipokuwa akizungumzia hali halisi ya watoto yatima katika Mkoa huo wa Iringa, kwenye warsha iliyoandaliwa na Shirika la Kimataifa la Kuwahudumia Watoto (UNICEF) hivi karibuni mjini Kibaha.
Bibi Mafuru amesema kuwa, utafiti uliofanywa kwa ushirikiano kati ya Shirika lisilo la Kiserikali la Uingereza la Family Health International, UNICEF na TAHEA umegundua kuwa wilaya ya Makete peke yake ina watoto yatima wapatao 13,000 hadi kufikia Juni mwaka 1998.
Bibi Mafuru amesema takwimu hizo pia zimeonyesha kuwa asilimia kubwa ya vifo katika wilaya hiyo huwa ni wanaume ambao wengi wao wamekuwa wakitelekeza wake zao pamoja na watoto na kwenda katika mikoa mingine yenye mashamba makubwa kama vile Kagera kutafuta kazi.
Asilimia 90 ya watoto yatima wameondokewa na baba zao na asilimia 10 tu ya watoto yatima wameondokewa na mama zao.
Aidha Mafuru amesema utafiti wao huo pia umebainl kuwa, robo tatu ya wakazi wa wilaya hiyo ya Makete ni wanawake kwa vile wanaumewengi aidha wamefariki ama kutoweka katika vijiji vyao kwa miaka kadha kwa ajili ya kwenda kutafuta maisha.
Naye Mratibu wa Family Health International, Bwana Christopher Mushi amesema utafiti wa awali uliofanywa na Shirika hilo umeonyesha kuwa wilaya ya Makete inakabiliwa na tatizo kubwa la ajira kutokana na kutokuwepo kwa viwanda ama mashamba ambayo yangeweza kutoa ajira.
Hii ndiyo sababu kubwa inayofanya wanaume wengi wa Makete hasa vijana kuondoka na kwenda kutafuta maisha sehemu nyingine, anasema bwana Mushi.
Amesema wakazi hao wa Makete wameiomba Serikali kuangalia upya uwezekano wa kufufua vitega uchumi na kuimarisha miundo ikiwepo pamoja na kuweka vivutio ili kuwafanya vijana wabaki na kuepuka tatizo la UKIMWl.
Chanzo cha UKIMWI katika wilaya hiyo ni hicho na kama vijana watabaki na kuishi na familia zao basi huenda ikaleta mafanikio katika vita dhidi ya Ukimwi.

Taswira